Baraza
la Udhibiti wa Vyuo vya Ufundi nchini Tanzania NACTE imekifungia chuo
cha Biashara, Mifugo na Kilimo cha Mbeya Polytechnic kwa kushindwa
kukidhi vigezo ikiwa ni pamoja na kudahili wanafunzi wasio na sifa.
Akisoma
uamuzi huo kwa niaba ya NACTE, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Amosi Makalla
amesema kuwa taarifa kutoka NACTE zinaonesha kuwa chuo hichi kina
mapungufu mengi ikiwa ni pamoja na kutoa mafunzo ya mifugo ambayo
hayajathibitishwa na vyombo husika vya serikali.
Pia
amesema kuwa chuo hicho kimekuwa kikidahili wanafunzi wasiokuwa na
vigezo, akitolea mfano wanafunzi wanaosoma kozi ya mifugo ambapo kati ya
wanafunzi 359 ni wanafunzi 89 pekee ndiyo wanaotambulika kuwa na vigezo
husika.
Wakizungumza
kwa uchungu baadhi ya wanafunzi wamelalamikia chuo hicho kwa
kuwasababishia upotevu wa muda na gharama, ambapo baadhi yao walikuwa
tayari wamehitimu na walikwenda chuoni hapo kufuatilia vyeti.
“Mimi
nimetoka mbali, nimekuja kufuatilia cheti changu, sasa nina miezi
miwili hapa, kila siku nazungushwa nazungushwa, kumbe walijua wanakuja
kufungiwa, kwahiyo cheti changu sipati, na muda nimepoteza, nimekaa hapa
miaka mitatu halafu leo naambiwa miaka yangu mitatu haina maana tena,
sikubali sikubali..” amesema mwanafunzi Catherene Buda
Kwa upande wake Mkurugenzi wa chuo hicho Ellertoni Mwamasika, ameomba radhi na kusema kazi ya kuendesha chuo ni ngumu “Chuo kinawaomba radhi wote, ila mjue kuwa kazi hii ya kuendesha chuo ni ngumu”
Hata
hivyo serikali imesema wanafunzi wenye sifa watahamishiwa katika vyuo
vingine huku ikimuagiza mmiliki wa chuo hicho kuwalipa wanafunzi gharama
zao zote kabla hawajatoka chuoni hapo.
Post your Comment



