KATIKA kukabiliana na suala la rushwa na ufisadi, serikali imetenga
jumla ya Sh bilioni 2.5 ili kuwezesha uanzishwaji wa Mahakama ya
Mafisadi. Aidha, serikali imetenga jumla ya Sh bilioni 72.3 katika
bajeti ya mwaka 2016/17 kwa ajili ya shughuli mbalimbali za Taasisi ya
Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) ili kuiwezesha taasisi hii
kutekeleza majukumu yake kikamilifu.
Hayo yamo katika Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2016/17,
iliyowasilishwa bungeni mjini Dodoma jana na Waziri wa Fedha na Mipango,
Dk Philip Mpango. Katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi
(CCM), iliweka wazi kwamba itaanzisha mahakama maalumu ya kukabiliana na
mafisadi na wahujumu wa uchumi, na hivi karibuni Waziri Mkuu, Kassim
Majaliwa alitangaza kwamba mahakama hiyo itaanza Julai mosi, mwaka huu.
Dk Mpango alisema vile vile katika bajeti ya mwaka 2016/17, serikali
imetenga Sh bilioni 44.7 kwa ajili ya kuiwezesha Ofisi ya Taifa ya
Ukaguzi (NAO) kutekeleza majukumu yake ya msingi ya kukagua na kudhibiti
matumizi ya fedha za umma.
Post your Comment



