Balozi wa
kujitolea wa mazingira, Omary Kombe ameiomba Serikali kuwatambua watu
wanaobadilisha taka kuwa bidhaa kwa kuendeleza taaluma hiyo ili kuinua uchumi
na kuondokana na tatizo la uchafu nchini.
Akiongea na waandishi wa habari Mei 18, 2016 jijini Dar es Salaam, Kombe alisema kwamba kwa kuwatambua watu hao, tatizo
la taka litakwisha kwa kiwango kikubwa nchini hasa katika jiji la Dar es
Salaam.
“Wapo watu ambao mara nyingi tunawaona
kwenye maonyesho mbalimbali kama vile sabasaba ambao wanauwezo wa kubadili taka
kuwa bidhaa za majumbani kwa mfano, mkaa, mapambo na bidhaa nyingine, ni vizuri
Serikali ikawatumia watu hao kuondokana
na tatizo la taka nchini,” alisema Kombe.
Aliongeza kwamba, mazingira bado ni
machafu licha ya serikali ya awamu ya tano kuweka mkazo katika suala zima la usafi kuanzia ngazi
ya familia mpaka Taifa ili kukabiliana na magonjwa ya mlipuko kama vile kipindupindu.
Kombe alisema kwamba, tatizo hilo la
uchafu litatatuliwa kama watu wenye uwezo wa kubadilisha taka kuwa bidhaa
watatambuliwa na kufanya kazi hiyo kuwa rasmi.
Aidha alisema kuwa, kwa kubadilisha
taka kuwa bidhaa kutapunguza kiwango cha taka nchini, kuongeza ajira pamoja na kuipunguzia Serikali mzigo wa kutenga maeneo
kwa ajili ya kuhifadhia taka kila mara.
Usafi ni kauli mbiu ambayo imeshika
kasi awamu hii ya tano ambapo katika sherehe za Uhuru (Tisa Desemba) Rais Dkt.
John Pombe Magufuli aliwataka watanzania wote kushiriki usafi maeneo yanayowazunguka
na vituo vya jamii kama hospitali, zahanati na vituo vya afya.
Post your Comment



